Visa vya dhuluma dhidi ya watoto vimekidhiri. Kwenye vyombo vya habari kila kutwa utasikia kuhusu hao waliokosa nidhamu kwa kuwadhulumu malaika wachanga wasio na hatia. Baadhi yao ni walimu waliopatiwa majukumu ya kuwanoa watoto, wazazi wanaopaswa kuwalea na kuwalinda au majirani wanaofaa kuwa wahisani kwa watoto hao. Wengine ni watu wa kila aina wasioona haya kutekeleza maasi sampuli hiyo.

Kwenye shairi lifuatalo kifaranga analalamika kwa jogoo. Anamwonya na kumwagiza asubiri hadi awe mtamba kwa kuwa udogoni hamfaidi kwa lolote. Kifaranga huyu analinganishwa na mtoto asiye na hatia anayemweleza mhuni asimtendee maovu bali amsubiri hadi ukubwani. Shairi lenyewe ni nasaha na onyo kwa binadamu aliye na wazo potovu la kumwangamiza mtoto, hasa wa kike, kwa kumdhulumu kimapenzi. Subiri Niwe Mtamba


Subiri Niwe Mtamba

Kokoriko sijaimba, ningali sijawa nyuni,
Makanyagio yayumba, ukubwa sina sinani,
Sidonoi hata tumba, henitoshi kidonani,
Subiri niwe mtamba, kifaranga nafaani?

Najizoesha kutamba, mwewe selea angani,
Wanisaka kwa kizimba, miye wanitakiani?
Hujaola yangu gumba, uniache salimini,
Subiri niwe mtamba, kifaranga nafaani?

Jimbi umekuwa mamba, unimege udogoni,
Wanivuta twende chemba, unidone faraghani,
Usinifunge kwa kamba, unitwae mafichoni,
Subiri niwe mtamba, kifaranga nafaani?

Kikwara unanikemba, udogo wangu huoni,
Wahaka umenikumba, nikuonapo chumbani,
Kuenda kwenye shamba, wanifata u mbioni,
Subiri niwe mtamba, kifaranga nafaani?

Kunifata wanitimba, uniache mchangani,
Kama ngozi waniwamba, uchafu unisheheni,
Hishimu aleniumba, nitotolewe yaini,
Subiri niwe mtamba, kifaranga nafaani?

© Kimani wa Mbogo (15/04/2010)

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *

*