Tujifunzayo ni mengi, tuingiapo shuleni,
Marafiki wangu wengi, twacheza nao nyanjani,
Twaongea mambo mengi, lugha moja twaighani,
Kiswahili kitukuzwe, lugha yetu ya taifa.
Kuongea Kiswahili, tumia lugha sanifu,
Ufasaha wa ukweli, tukuze kwa ukunjufu,
Hili langu ukubali, tuupate usanifu,
Kiswahili kitukuzwe, lugha yetu ya taifa.
Lugha sanifu iwepo, Kiswahili tukikuze,
Ufasaha upendapo, nalo pengo ulijaze,
Popote utembeapo, watu wote waeleze,
Kiswahili kitukuzwe, lugha yetu ya taifa.
Darasani uiseme, lugha yetu ya heshima,
Japo taenda uhame uendako yawe mema,
maneno yote useme, kwa wema na lugha njema,
Kiswahili kitukuzwe, lugha yetu ya taifa.
© Kimani wa Mbogo (01/01/2007)