Endapo awe mtumwa, mdukizi asemeni?
Aliseme lisosemwa, ujumbe kuwapasheni,
Mtimani ataumwa, ukweli awambieni,
Mbasi wa mdukizi, hana budi kudukiza.
Fitina ataitia, rafikiyo ukidhani,
Mabaya takutakia,ukisema ni mwandani,
Mwishowe utawadia, utakuwa mfitini,
Mbasi wa mdukizi, hana budi kudukiza.
Usipojichunga naye, utabaki mdukizi,
Lolote akuambiye, utasema ni azizi,
Masaibu yakujiye, uanzapo udakizi,
Mbasi wa mdukizi, hana budi kudukiza.
Kikulacho ki nguoni, kikwandamacho kibovu,
Kikunywacho ki mwilini, kikwendeacho uovu,
Kikuacho ki tumboni, kikwekacho ulegevu,
Mbasi wa mdukizi, hana budi kudukiza.
Chema ndicho chajiuza, tajiuzaje mdaku?
Kibaya chajitembeza, kitembee kila siku,
Endelea kudukiza, wonekane kama kuku,
Mbasi wa mdukizi, hana budi kudukiza.