Arudhi katika fasihi ni sehemu muhimu katika elimu ya utunzi wa mashairi. Hasa arudhi inaelezea vipengele vya mashairi kama beti, idadi ya mishororo, vina na mizani. Shairi ni Arudhi


Shairi ni Arudhi

Msiziwanie hadhi, mkibusu ufahari,
Huenda mkabughudhi, magwiji wa ushauri,
Walisema heri radhi, mali sana huwa shari,
Pasipokuwa arudhi, tungo haiwi shairi!

Hata upambe lafudhi, kwa lahaja ziwe shwari,
Wasomao utaudhi, usipofata bahari,
Tungo za haja kukidhi, zazuia kushamiri,
Pasipokuwa arudhi, tungo haiwi shairi!

Zipashe hizo nyaadhi, ila muhimu urari,
Wadai yetu upudhi, kaamua kughairi,
Hizo walitukabidhi, ndizo zenye uhodari,
Pasipokuwa arudhi, tungo haiwi shairi!

La kuitwa mfawidhi, si maana kufahiri,
Utungayo ni maradhi, kupooza ushairi,
Iwate hiyo ghaidhi, uanze kutafakari,
Pasipokuwa arudhi, tungo haiwi shairi!

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *

*