La wazi nimetambuwa, hakika nikabaini,
Dhahiri nimeelewa, likanijaa wazoni,
Lilo muhimu si dawa, amani kuwa moyoni,
Licha yako kutibiwa, hunalo la afueni!
Mafumbo tumetatuwa, mengi tuliyoyadhani,
Mashakani umetiwa, ni ugonjwa si utani,
Mbio umetimuliwa, ukaisha ukingoni,
Licha yako kutibiwa, hunalo la afueni!
Kiwewe umeingiwa, kudhoofika mwilini,
La fahamu kupotewa, udhaifu ubongoni,
Waganga wa kuswifiwa, hawanalo kubaini,
Licha yako kutibiwa, hunalo la afueni!
Kwa muda umeuguwa, tena ikawa huponi,
Maradhi kujitanuwa, vema yakakubaini,
Haya yamekubambuwa, ukawa huna hunani,
Licha yako kutibiwa, hunalo la afueni!
Wauguzi kapagawa, hawanalo la makini,
Kuganga na kuganguwa, limekwama maishani,
Ni mengi yameshakuwa, si machache ulodhani,
Licha yako kutibiwa, hunalo la afueni!
Ningependa kupata haya mashairi
Jiunge nasi kwenye channel ya Telegram: https://t.me/mwanagenzimtafiti