Mapenzi ni jambo la mtu na hiari yake. Hulazimishwi kumpenda huyu ama yule. Wengine watakuvunja moyo na kukwambia unayempenda si mwema. Kila mtu ana ila zake. Hakuna mwanadamu aliye kamili asilimia mia moja. Unapozitambua ila za mke wangu, jua na usinipashe kwa kuwa nilizijua kitambo. Wengine watakupasha mengi yasiyo na maana wala ukweli kuhusu mpenzi wako ili umwache amtongoze. Mara nyingi udaku hupotosha na kuangamiza wawili wapendanao ama hata familia.

Shairi lifuatalo la tarbia lina mengi ya kufahamisha. “Sijali mnavyomwita, kwangu huwa maridhia”. Hata mseme, mmbadike majina ama mmdharau, kwangu nampenda tu. Mpenzi wa mtu ni mpenzi wake tu yawache ya kwao huyawezi. Hebu lisome na utafari kwa kina. Ufurahiae uhondo wa shairi hili la Kimani wa Mbogo analoliita “Kwangu huwa maridhia”. Kwangu Huwa Maridhia


Kwangu Huwa Maridhia

Hamnazo mwajitia, nipendaye mwabubuta,
Vya wengine mwasifia, kilicho chake mwabeta,
Lawama mnamtia, ikawa mnamsuta,
Sijali mnavyomwita, kwangu huwa maridhia.

Mema yanapowadia, mwaona yenu yasita,
Lake mwaita hatia, kwa yenu mnajibwata,
Mwadhani mmetimia, mkajiona mwakita,
Sijali mnavyomwita, kwangu huwa maridhia.

Dada yuwalialia, amebaki akibweta,
Tanuri ameingia, mtashangaa kupita,
Thamani mwakadiria, msijue awaketa,
Sijali mnavyomwita, kwangu huwa maridhia.

Maovu mwamtajia, dada mwamkereketa,
Lake hamjasikia, moyo mnavyofukuta,
Pale mnapopitia, kutwa mtajikunyata,
Sijali mnavyomwita, kwangu huwa maridhia.

Kwa mengi mwajisikia, ati bongo amenata,
Majina mwampatia, hamna radhi kumwita,
Laana mwamtakia, kumwingiza kwa matata,
Sijali mnavyomwita, kwangu huwa maridhia.

Yenu sitakubalia, mtakavyo kumng’ata,
Matusi kumvamia, si jambo la kumgota,
Sasa mnafurahia, vibaya kumkong’ota,
Sijali mnavyomwita, kwangu huwa maridhia.

Adhabu itasalia, vitukuu kufuata,
Mungu atamjalia, kwa huo wake utata,
Yote mnamfanyia, yanamfanya kukita,
Sijali mnavyomwita, kwangu huwa maridhia.

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *

*