Kwa sasa ninayo hoja, hata kama ya uchungu,
Nimeviona viroja, vinavyokutia pingu,
Maswahibu huna haja, umepotea mwanangu,
Figa hilo lako moja, litainjikaje chungu?
Twajua wako uteja, wenendako wanguwangu,
Maneno unayotaja, yamekithiri mizungu,
Kwa jamii wajichuja, huthamini hata Mungu,
Figa hilo lako moja, litainjikaje chungu?
Mambo kweli ni kangaja, huja pia kwa mikungu,
Unahitaji daraja, kivuko kama cha pungu,
Kwa wanadamu hujaja, wajificha kwa vitangu,
Figa hilo lako moja, litainjikaje chungu?
Litakwalo ni umoja, ili pako pawe pangu,
Umezidiwa na luja, ukabadilika bungu,
Ishi vema nao waja, usiishi zako mbingu,
Figa hilo lako moja, litainjikaje chungu?
Hiyo yako si faraja, ni mateso chunguchungu,
Uzipatapo wafuja, unenewapo u nungu,
Upatacho wabigija, ukituonesha tungu,
Figa hilo lako moja, litainjikaje chungu?