Sina mengi ya kufanya, niendapo sebuleni,
Nikaliapo foronya, nyoyo zangu sakafuni,
Peremende namumunya, utamu mwingi kinywani.
Kachi nikishakalia, nakaribia mezani,
Kwa swichi nafungulia, redio kwanza uneni,
Mengi inanipashia, kupitia sikioni.
Nasikia matangazo, toka yangu redioni,
Mambo mengi na mawazo, yaingia ubongoni,
Yakitiliwa mkazo, nasikiza kwa makini.
Muziki unapovuma, nasimama sakafuni,
Nacheza nikiwa wima, peke nikiwa chumbani,
mdundiko ni wa ngoma, kusikiza redioni.
Maonyo huwa si haba, kusikia redioni,
Aniambiavyo baba, kutoka mwake kinywani,
Hujua dawa ya tiba, nikiwa bado nyumbani.