Raha hupendelewa, lewa utayumbayumba,
Yumba unapopagawa, gawa kosa usambamba,
Amba bila kuelewa, lewa wende ukiimba,
Imba nitajivunia, nia yangu ni furaha!
Raha yangu kuposana, sana nilipe mahari,
Ari hijakosekana, kana uitwe fakiri,
Kiri mwenyewe kijana, jana ulivyotabiri,
Tabiri tajivunia, nia yangu ni furaha!
Raha si kujidukiza, kiza ukapendelea,
Lea ukijitukuza, kuza unapotegea,
Gea uweke ruwaza, waza yanoendelea,
Elea tajivunia, nia yangu ni furaha!
Raha sio kutapia, pia sio kujisifu,
Sifu bila kutania, nia ya ufanikifu,
Kifu kaa kupalia, lia kwa mhalifu,
Alifu tajivunia, nia yangu ni furaha!
Raha sio patashika, shika ukajilaumu,
Laumu kwa kupotoka, toka nje tarakimu,
Kimu ukamemeteka, teka nyara tachodumu,
Dumu nitajivunia, nia yangu ni furaha!